Eriksen aiweka njia panda Spurs

Muktasari:

Spurs wanataka kumuongeza mkataba Eriksen huku wakitaka kumpa ofa ya mshahara wa Pauni 200,000 kwa wiki kutoka ule wa Pauni 80,000 kwa wiki

Tottenham Hotspur ipo tayari kumuongeza mshahara kiungo wao, Christian Eriksen ili aendelee kubaki katika klabu hiyo.

Pamoja na klabu hiyo kutoka kumuongezea dau bado kiungo huyo wa Denmark amewahi kusema fedha sio kitu kinachoweza kubadili uamuzi wake siku chache kabla ya kugoma kusaini mkataba mpya.

Spurs wanahitaji kumuongeza mkataba Eriksen huku wakitaka kumpa ofa ya mshahara wa Pauni 200,000 kwa wiki kutoka Pauni 80,000 kwa wiki.

Kwa mujibu wa vyanzo vya ndani nchini England, vinadai Eriksen anaweza kusaini mkataba huo wenye vipengele vya kumfanya aondoke muda wowote endapo ikitokea ofa ya maana.

Real Madrid na Juventus zinaonekana kummezea mate kiungo huyo majira haya ya kiangazi.

Mwenyekiti wa Totenham, Daniel Levy anaweza kumuuza Eriksen majira haya lakini uamuzi huo unaweza kukiathiri kikosi cha Mauricio Pochettino kutokana na dirisha la usajili nchini humo kufungwa huku kwa mataifa mengine ya Ulaya likiwa wazi hadi Septemba 2.

Eriksen alionyesha ubora wake kwenye mchezo uliopita kwa Spurs, Jumamosi ambapo aliiwezesha  timu hiyo kutoka nyuma na kuibuka  na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Aston Villa.