Griezmann aanza mazoezi Barcelona, Atletico yasema inakwenda FIFA

Muktasari:

Uhamisho wa mshambuliaji huyo wa Ufaransa umekumbwa na utata kuhusu muda ambao alifikia makubaliano na Barcelona na ule wa kupungua kwa kiwango cha fedha za kumruhusu kuondoka.

Mshambuliaji wa Ufaransa, Antoine Griezmann leo amefanya mazoezi pamoja na wachezaji wa klabu yake mpya ya Barcelona kwa mara ya kwanza baada ya uhamisho wake uliokuw na utata.

"Sehemu ya kwanza kati ya mbili za mazoezi ilimalizika kwa wachezaji wote wa kikosi cha kwanza kuhudhuria, wakiwemo wapya kabisa ambao ni Frenkie de Jong, Neto, na Antoine Griezmann," klabu bhiyo ya Catalanya inasema kwenye tovuti yake.

Mshambuliaji mwingine wa Ufaransa, Ousmane Dembele, na kipa Mjerumani Marc-Andre Ter Stegen wote walitangazwa kuwa wako katika hali nzuri kiafya baada ya kupona majeraha waliyopata msimu uliopita.

Lakini hakukuwepo na dalili za Lionel Messi, Luis Suarez, Philippe Coutinho, Arthur na Arturo Vidal ambao bado wako likizo baada ya kuzitumikia nchi zao katika fainali za Amerika Kusini (Copa Amerika).

Griezmann alitambulishwa kuwa mchezaji wa Barcelona Jumapili usku baada ya klabu hiyo kumlipia Mfaransa huyo dola 135 milioni zilizowekwa kwenye kifungu cha mkataba wake kama sharti la kumruhusu aondoke.

Atletico imeelezea kiwango hicho cha fedha kuwa hakitoshi, ikilalamika kuwa Barcelona na Griezmann walishafikia makubaliano kabla ya kifungu hicho fedha zilizowekwa kwenye kifungu hicho kupunguzwa kutoka dola 200 milioni mwanzoni mwa mwezi Julai.

Gazeti la michezo la Hispania, AS llisema Jumamosi kuwa Atletico itakwenda Shirikisho la Kimataifa la Soka (Fifa) kuidai Barcelona fedha zaidi ya dola 135 zilizolipwa na mwanasheria wa Griezmann Ijumaa.

Barcelona inakwenda Japan Jumamosi ambako itacheza mechi za kirafiki dhidi ya Chelsea Julai 23 na baadaye timu ya Andres Iniesta inayoitwa Vissel Kobe siku nne baadaye.