Manchester United yamtega nahodha Aston Villa

Muktasari:

Grealish mwenye miaka 24, amepewa jukumu la kuinusuru Aston Villa na janga la kuteremka daraja.

London, England. Manchester United imejiandaa kutoa Pauni 160 milioni kunasa saini za wachezaji wawili kwa mpigo akiwemo nahodha wa Aston Villa, Jack Grealish.

Pia Manchester United inataka saini ya mchezaji wa Leicester City, James Maddison. Kocha Ole Gunnar Solskjaer ameingia sokoni kusaka wachezaji katika majira ya kiangazi msimu ujao.

Solskjaer ana matumaini ya kuwapata wachezaji hao baada ya kumpiga bei kiungo Paul Pogba anayewindwa na Real Madrid, Juventus zinazomtaka katika usajili wa majira ya kiangazi.

Manchester United ilimsajili nahodha wa Sporting Lisbon, Bruno Fernandes katika usajili wa dirisha dogo mwezi uliopita.

Kocha huyo anataka kuisuka upya Man United baada ya msimu huu kupoteza matumaini ya kutwaa ubingwa na sasa anapambana kupata nafasi moja kati ya nne za Ligi Kuu England.

Maddison anapewa nafasi ya kutua Man United kutokana na uhusiano wake na kocha huyo raia wa Norway.

Grealish mwenye miaka 24, amepewa jukumu la kuinusuru Aston Villa na janga la kuteremka daraja baada ya timu hiyo kutopata matokeo mazuri.