Zahera: Siku tatu za Moro zimenipa mwanga

Muktasari:

  • Yanga inajiandaa na mchezo dhidi ya Simba utakaopigwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa

Morogoro. Kambi ya Yanga mkoani Morogoro imeongeza morali kwa wachezaji wake baada ya mbinu zote za uwanjani zilizopangwa kwenda kama ilivyotakiwa.

Kocha Mwinyi Zahera alisema katika mazoezi ya siku tatu ameweza kutengeneza programu ambazo zitawafanya wachezaji wake waweze kuibuka na ushindi katika mchezo wao dhidi ya Simba.

Zahera alisema katika siku yake ya kwanza alihakikisha anawaondolea uchovu wachezaji wake kwa kuwapa mazoezi mepesi ili wasiweze kupata fatiki.

"Wamecheza mechi nyingi mfululizo kwahiyo walihitaji mazoezi mepesi ili kuondoa mchoko wa mwili, tulifanikiwa katika hilo kwa asilimia kubwa," alisema.

Aliongeza kwamba siku yake ya pili alitumia kuwapa umakini wachezaji wake kuhakikisha kwamba muda wote macho yao yapo katika mpira na sio kitu kingine.

 

"Baada ya kuondoa uchovu tuligeukia katika umakini na mpira, tunatakiwa muda wote tuhakikishe kwamba tunacheza mpira, tukiukosa tunautafuta na kuwa nao tena," alisema.

Aliongeza kwamba anaamini mchezo huo utakuwa mgumu kwa timu zote kutokana na maandalizi ambayo wamekuwa wakifanya.