Roma ataja sababu za kwa nini hajarejea Tanzania

Muktasari:

  • Mwezi mmoja tangu msanii Roma kuachia nyimbo yake ya Anaitwa Roma msanii huyo amekuwa akiishi marekani hali ambayo imekuwa ikizua minongono ya kuwa anaogopa kurejea nchini Tanzania.

Nyota wa Hip Hop Nchini Tanzania anayetamba na wimbo  ‘Anaitwa Roma’ , Roma Mkatoliki amefunguka sababu za yeye kushindwa kurejea Tanzania kwa  wiki nne  tangu aende Marekani huku akikanusha taarifa za kuwa wimbo wake mpya  ndio sababu ya yeye kuogopa kurejea nchini.

Takribani mwezi sasa msanii huyo amekuwa nchini Marekani na kuonekana katika shughuli mbalimbali nchini humo hali ambayo iliibua maswali ya kwanini hajarejea nchii Tanzania .

Akizungumza na Radio Clouds Fm ya Tanzania leo Jumapili Desemba 15, 2019 Roma ameeleza kuwa sababu kubwa iliyompeleka marekani ni mualiko maalum alioupata kutoka kwa jamii ya watu wanaozungumza Kiswahili wanaoishi marekani maarufu kama SUSA (Swahili society USA) mualiko ambao ameeleza kuwa aliupata kama msanii wa Tanzania anayetumia Kiswahili katika kazi zake za kufikisha ujumbe kwa Jamii husika ambapo tamasha hilo hufanyika kila mwaka.

Roma ameeleza kuwa katika tamasha hilo alikuwa na wasanii wengine wa Tanzania ambao baadhi amewataja kama Masanja Mkandamizaji, Mr Beneficial, Bwana Mjeshi pamoja na wadau wengine wa kiswahili walioalikwa kushiriki kujadili faida za Kiswahili katika shughuli zao

Akizungumzia sababu za kuchelewa kurejea nchini Tanzania hata baada ya tamasha hilo kumalizika Roma amesema  kwa kuwa yeye ni kijana na anatafuta fursa kila mahali amepata nafasi ya kuangalia fursa zilizopo nchini humo.

 “US kuna fursa nyingi, unapozunguzia tasnia ya burudani huku ndio kama mama, kiukweli  sio sehemu ya kuja Jumatano alafu Alhamisi ukaondoka, kuna fursa nyingi, kuna watu wetu, mashabiki wetu ambao sjawahi kuwaona ni mara yangu ya kwanza kufika huku, kwahiyo utajikuta una vitu vingi vya kufanya” ameeleza Roma wakati akihojiwa na Radio Clouds Fm ya Tanzania.

Aidha Roma amesema kuwa bado yeye ni kijana hivyo kuna shughuli nyingine binafsi pia anaweza kuzifanya huko ikiwa ni pamoja na kutumia sanaa yake kuitangaza nchi ya Tanzania

Kuhusu tetesi za kwamba wimbo ndio chanzo cha yeye kushindwa kurejea Tanzania Roma amesema kuwa wanaosema hivyo hawamjui sababu amekuwa na utaratibu wa kuachia nyimbo zake akiwa nje ya nchi kila.

 “Nilishatangaza tangu tunaachia nyimbo ya kijiwe Nongwa kuwa huu mwaka hautaisha kabla ya Roma na stamina kuachia Solo Project zao tuliweka wazi mapema, so wakati niko huku (Marekani) nikaona ni wakati mzuri wa kuachia wimbo, so wanaosema Roma aliachia wimbo wa anaitwa Roma alafu akakimbilia marekani sio kweli” amesema Mkali huyo wa HipHop aliyewahi kutikisha afrika kwa tukio la kutekwa kwake.