Shahidi akwamisha usikilizaji kesi ya meno ya tembo

Raia wa China, Young Feng Glan (wa pili kulia),  anayeshitakiwa kwa makosa ya  usafirishaji vipande zaidi ya 700 vya meno ya tembo, akiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam. Picha na Maktaba

Muktasari:

Hakimu ameahirisha kesi kutokana na shahidi wa upande wa mashtaka kuwa na udhuru.

Dar es Salaam. Kesi ya uhujumu uchumi kwa kujihusisha na meno ya tembo yenye thamani ya Sh13 bilioni itaendelea kusikilizwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kesho, Oktoba 18, 2017.

Wakili wa Serikali, Paul Kadushi leo Jumanne amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa ilipaswa kuendelea kusikilizwa lakini shahidi wa upande wa mashtaka amepata udhuru.

Baada ya kueleza hayo, wakili wa utetezi, Nehemiah Nkoko amesema alitarajia upande wa mashtaka ungeandaa mashahidi wawili au watatu ili mmoja akipata udhuru wengine waendelee.

Nkoko ameutaka upande huo kuandaa mashahidi watatu ili hali kama hiyo isijitokeze kesho.

Hakimu Shaidi ameuagiza upande wa mashtaka kuzingatia suala hilo na ameahirisha kesi hadi kesho kwa ajili ya kuendelea na usikilizwaji.

Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa mfululizo kuanzia Oktoba 18, 19 na 20, mwaka huu.

Washtakiwa Salvius Matembo, Philemon Manase na raia wa China anayedaiwa kuwa Malkia wa Pembe za Ndovu, Yang Feng Glan (66), wanakabiliwa na kesi ya kuhujumu uchumi kwa kujihusisha na meno ya tembo yenye thamani ya Sh13 bilioni.

Washtakiwa wanadaiwa kati ya Januari Mosi, 2000 na Mei 22, 2014  walijihusisha na biashara  ya nyara za Serikali kinyume cha sheria.

Washtakiwa wanatetewa na mawakili Nkoko, Hassan Kihangio na Jeremiah Mtobesya.