Uraia wa watu waliokuwemo kwenye ndege iliyopata ajali watambuliwa

PICHA KWA MSAADA WA | TIKSA NEGERI | REUTERS

Muktasari:

Ajali hiyo imetokea leo  asubuhi baada ya  ndege hiyo kupoteza mawasiliano na kuanguka katika mji wa Bishoftu uliopo kilomita 60 kutoka Kusini Mashariki mwa Addis Ababa kwa njia ya barabara

Addis Ababa,Ethiopia. Shirika la Ndege la Ethiopia limetaja raia na mataifa ya watu waliopata ajali, kwenye ndege ya shirika hilo iliyotokea asubuhi ya leo.

Kwa mujibu wa taarifa ya shirika la ndege la Ethiopia, ndege hiyo iliruka saa 2:38 asubuhi kwa saa za Ethiopia kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Bole na kwamba watu waliokuwemo ndani ya ndege hiyo wanatoka katika nchi 33.

“Kwa wakati huu, operesheni ya utafutaji na uokoaji miili zinaendelea na hatuna taarifa zilizothibitishwa za waliopona au waliojeruhiwa kwenye ajali hii. Wafanyakazi wa shirika hili wamekwenda eneo la tukio na watafanya kila linalowezekana kutoa huduma za dharula,” inasomeka sehemu ya taarifa ya shirika hilo.

Msemaji wa Shirika hilo, Asrat Begashaw alinukuliwa na Shirika la Habari la Kitaifa la Ethiopia akithibitisha kwamba hakuna abiria hata mmoja aliyenusurika katika ajali hiyo, wote wamekufa.

Kampuni hiyo inasema imeanzisha kituo cha kupata taarifa kuhusu familia na marafiki za watu waliliokuwemo ndani ya ndege hiyo.

Alitaja  mataifa na idadi ya raia waliokuwepo kwenye ajali hiyo kwamba ni pamoja na Wakenya (32), Wacanada ( 18) , Waethiopia ( 9) Wachina (8), Waitaliano ( 8), Wamarekani ( 8) Waingereza ( 7), Wafaransa (7), Wamisri ( 6), Waholanzi ( 5), Wanadiplomasia wa UN( 4).

Amesema mataifa mengine ni  Wahindi ( 4) Warusi ( 3), Wamorocco ( 2), Waisraeli ( 2) na ubelgiji, Uganda , Yemeni, Sudan  , Togo , Msumbiji pamoja na  Norway  kuwakiwa na raia mmoja mmoja.

 Abiria 149 pamoja na wafanyakazi wanane wa ndege aina ya Boeing 737 ya Shirika la ndege la Ethiopia wamefariki baada ya ndege hiyo kuanguka dakika sita baada ya kupaa kutoka Addis Ababa kwenda Nairobi, Kenya.