Chadema yalaani polisi kumshikilia Halima Mdee

Muktasari:

  • Mapema leo asubuhi Halima Mdee aliitikia wito kutoka Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Makosa ya Jinai (RCO) Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, kufika Kituo cha Polisi Oysterbay kwa ajili ya mahojiano.
  • -Mdee amehojiwa kwa tuhuma za kutoa kauli za uchochezi kwenye moja ya mikutano yake ya hadhara aliyoifanya Jimbo la Kawe, ikiwa ni mwendelezo wa ratiba ya ziara za kuwatembelea, kuwasikiliza na kuwapatia mrejesho wapiga kura wake jimboni humo.

Dar es Salaam. Chama Kikuu cha Upinzani nchini Tanzania cha Chadema kimelaani hatua ya Polisi jijini Dar es Salaam kuendelea kumshikilia mbunge wake wa Kawe, Halima Mdee.

Mdee ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha) anashikiliwa katika Kituo cha Polisi Oysterbay alikofika leo asubuhi Jumamosi Februari 23,2019 kwa mahojiano.

Mbunge huyo anashikiliwa kwa tuhuma za kutoa lugha za kichochezi katika moja ya mikutano yake aliyoifanya jimboni mwake hivi karibuni.

Taarifa ya Chadema iliyotolewa leo Jumamosi na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano, Tumaini Makene imesema imewaagiza wanasheria wake kuhakikisha mapema Jumatatu Februari 25,2019 wanaandika hati ya kuomba Mdee afikishwe Mahakama Kuu au aachiwe.

Chadema pia kupitia taarifa hiyo kimelaani na kukemea vikali kitendo hicho cha polisi ambacho ni ukiukwaji wa wazi wa haki za binadamu.

Taarifa hiyo imesema huo ni  mwendelezo wa vitendo vya jeshi hilo maeneo mbalimbali nchi nzima, kuwatendea wapenzi, wafuasi, wanachama na viongozi wa Chadema kinyume na taratibu za sheria za nchi.

“Chama kinachukulia tukio hilo la leo kuwa ni kuendelea kuandamwa kwa wawakilishi wa Chadema wenye nafasi za kiserikali, wakiwemo wenyeviti wa serikali za mitaa, madiwani na wabunge, wanapokuwa wakitekeleza majukumu yao, likiwa limetokea siku chache baada ya Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi 'Sugu' kuhojiwa na kushikiliwa na polisi kwa kutimiza wajibu wake,” imeeleza taarifa hiyo.

 

 

Kupitia taarifa hiyo Chadema imeiomba Mahakama Kuu itoe amri ya kuwaita na kuwahoji polisi kwa kumshikilia Mdee na kumnyima dhamana, huku ikivitaka vyombo vya dola, hususan Jeshi la Polisi kuacha kutekeleza majukumu yake bila kuzingatia Katiba na sheria za nchi. 

 

“Haki ya kupata dhamana iko kwa mujibu wa sheria zetu. Haitolewi kwa utashi wa mtu wala mamlaka yoyote. Tunalikumbusha jeshi hilo kuwa kuminya na kunyima uhuru wa mtu kwa kumuweka ndani ni uonevu usiokubalika, unaostahili kupingwa, kukemewa na kulaaniwa vikali na watu wote wapenda haki, ”ilisema taarifa hiyo.