Dk Bashiru atoa kauli wabunge CCM wachapakazi, wazembe

Muktasari:

  • Katibu Mkuu wa chama tawala nchini Tanzania (CCM), Dk Bashiru Ally leo alikuwa mgeni rasmi kushuhudia utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/20 jimboni kwa Angelina Mabuna wa Ilemela ambapo ametumia fursa hiyo kutoa  onyo kwa wabunge wazembe kwamba hawatopata nafasi katika uchaguzi ujao huko wachapakazi akiwatangazia ahueni.

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa chama tawala nchini Tanzania (CCM), Dk Bashiru Ally amesema hatoshangaa wabunge wa chama chake kupitwa bila kupingwa wakati wa mchakato wa ndani wa kuwachagua wagombea watakaopeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao 2020.

Dk Bashiru ameyasema hayo leo Jumanne Julai 30, 2019 wilayani Ilemelea mkoani Mwanza wakati akizungumza katika mkutano wa kuangalia utekelezaji wa Ilani ya CCM jimbo la Ilemela linaloongozwa na Angelina Mabula ambaye pia ni Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara, Dk Bashiru ambaye pia ni mlezi wa mkoa wa Mwanza amesema hategemei wakazi wa Ilemela kufanya kosa kwa kuwa mbunge wao Angelina Mabula anafanya kazi nzuri.

“Sitashangaa kama akipita bila kupingwa, sitashangaa kwa wabunge wengi na madiwani wengi kupita bila kupingwa. Na sio kwamba nampigia kampeni hapana yeyote na aje ila ajue kwamba kiti kimekaliwa na aliyekalia ameenea. Ole wake mtu anayetaka mlango wa nyuma, hatutaki fujo kwenye chama chetu tunataka utulivu.”

“Wapo watakaosema tunaua demokrasia ndani ya chama, demokrasia ni maridhiano tukishakubaliana ndani ya chama, wewe endelea na mambo yako kwenye chama chako,” amesema Dk Bashiru

Katibu Mkuu huyo pia amesisitiza kwamba chama hakitawabeba viongozi walioshindwa kutimiza majukumu yao na kukiangusha chama.

“Tunatoa ulinzi kwa aliye chapa kazi sio mzembe anayetaka kubebwa maana hata ukibebwa kwenye mbeleko lazima ukae kwa adabu vinginevyo utadondoka,” amesema