Magufuli ampa kila mchezaji wa Stars kiwanja

Muktasari:

  • Rais John Magufuli ametoa zawadi ya viwanja mjini Dodoma kwa wachezaji wote wa timu ya taifa pamoja na bondia Hassan Mwakinyo na mwalimu wake

Dar es Salaam. Rais John Magufuli ametoa zawadi ya viwanja vya kujenga nyumba kwa wachezaji wote wa Taifa Stars pamoja na bondia Hassan Mwakinyo pamoja na mwalimu wa bondia huyo.

Kutokana na agizo hilo, Rais Magufuli alimuagiza Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kusimamia agizo hilo kwa kutafuta eneo zuri katika mkoa wa Dodoma ambako ni makao makuu ya nchi.

Ameyasema haya leo Jumatatu ya Machi 25, 2019 Ikulu jijini Dar es Salaam katika hafla ya kuwapongeza wachezaji wa timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) pamoja na bondia Hassan Mwakinyo baada ya kuiwakilisha vizuri nchi katika mashindano.

“Kama tumeweza kuwapatia mabalozi viwanja, hatuwezi kushindwa kuwapatia mabalozi mnaoiwakilisha nchi hii katika machuano mbalimbali viwanja vya kujenga,” amesema Magufuli.

Amesema ana uhakika kupitia mapato kidogo wanayopata katika shughuli zao watayatumia katika kuendeleza viwanja hivyo ili iwe historia kwa wachezaji hao wanaoiwakilisha nchi katika michuano mikubwa.

“Wanapostaafu, miguu inapokataa kupiga mipira, maisha yao yasiwe ya ajabu. Kwa kushirikiana na katibu mkuu mchukue majina yao, pamoja na Mbwana Samatta ambaye ameondoka jana usiku msimsahau, na hicho kiwanja ukiamua kukiuza ni shauri yako,” amesema Magufuli na kuongeza, “lakini nataka sisi kama Serikali kwa niaba ya Watanzania iwe kama shukrani yetu kwenu.”