Mahabusu 17 watoroka wakiwa mahakamani

Muktasari:

Mahabusu 17waliofikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Geita wakikabiliwa  na mashtaka mbalimbali wametoroka

 

Geita. Mahabusu 17waliofikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Geita wakikabiliwa  na mashtaka mbalimbali wametoroka.

Mahabusu hao walikuwa wamewekwa  katika ukumbi wa jengo jipya la mahakama wakisubiri kusomewa kesi zinazowakabili wametoroka Jumanne Mei 21, 2019.

Taarifa zilizolifikia Mwananchi zinaeleza kuwa  walitumia moja ya milango iliyokuwa katika jengo jipya la mahakama na kutoroka wakati askari wakiwa nje ya lango kuu la kuingia katika ukumbi huo.

Mkuu wa Magereza Mkoa wa Geita, Kamishina Msaidizi wa Magereza (ACP), Robert Rumanyika akizungumzia tukio hilo amesema jeshi hilo halijaanza utaratibu wa kuwapeleka mahabusu mahakamani kama ilivyo kwa mikoa mingine na kwamba kwa sasa mahabusu wanaopelekwa mahakamani wanakuwa chini ya uangalizi wa Jeshi la Polisi.

Alipoulizwa kuhusu jambo hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita,  Mponjoli Mwabulambo amesema ni kweli wametoroka.

Amesema kwa sasa hawezi kuzungumzia tukio hilo kwa undani kwa maelezo kuwa yupo katika ziara ya ufunguzi wa masoko ya dhahabu wilayani Geita, akiahidi kutoa ufafanuzi atakaporejea ofisini.

Endelea kufuatia Mwananchi kwa taarifa zaidi