Makonda amzungumzia Meya wa Chadema mbele ya Rais Magufuli

Muktasari:

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema Meya wa jiji Isaya Mwita yuko katika hatua za mwisho ili aweze kurudi CCM kwa sababu bila kufanya hivyo hatakuwa na uhakika wa kupata nafasi alizonazo sasa akiwa Chadema.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema Meya wa Jiji hilo, Isaya Mwita anayetokana na Chadema yuko katika maandalizi ya kuaga udiwani na umeya kwa sababu anajua bila kuwa CCM ni ngumu kurudi katika nafasi hizo.

Ameyasema hayo leo Juni 25, 2019 katika uzinduzi wa taifa Gesi unaofanyikia Kigamboni jijini Dar es Salaam ambapo Rais John Magufuli ndiyo mgeni  rasmi.

Makonda amesema katika kata anayoongoza Mwita kuna shule iliyokuwa na wanafunzi 3,764 lakini walimu walikuwa wanakaa chini huku Meya huyo akiendelea kupeperusha bendera.

“Nikamuambia walimu wa Dar es Salaam hawawezi kukaa chini hapa, sasa tumeshawapa ofisi wanakaa vizuri na Mstahiki Meya (Mwita) anajiandaa kiukweli kurudi kule kunakostahili,” amesema Makonda.

Hii si mara ya kwanza kwa Makonda kumzungumzia Meya Isaya katika hafla mbalimbali zinazofanyika jijini humo na kuhudhuriwa na Rais Magufuli na meya mwenyewe na nyakati zingine aliwahi kusema yuko Chadema lakini anatekeleza ilani ya CCM.