Makonda awatangazia vita wamachinga wasio na vitambulisho

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amewataka wamachinga  wanaofanya shughuli zao katika Jiji hilo bila kuwa na vitambulisho vya wafanyabiashara wadogo kuwa navyo kabla ya Juni 3, 2019

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amewataka wamachinga  wanaofanya shughuli zao katika Jiji hilo bila kuwa na vitambulisho vya wafanyabiashara wadogo kuwa navyo kabla ya Juni 3, 2019.

Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Mei 29, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari kuhusu mwitikio wa wafanyabiashara kuchukua vitambulisho hivyo vilivyotolewa na Rais John Magufuli kwa wakuu wote wa Mikoa nchini.

Katika maelezo yake Makonda amesema Jiji hilo lilipatiwa vitambulisho 175,000 lakini wapo ambao hawajachukua hadi sasa.

“Nimefanya utafiti kwa kuzunguka mitaa tisa ambayo shughuli za ujasiriamali zinafanyika lakini cha ajabu wamachinga wengi hawana vitambulisho hivi.”

“Hadi Jumatatu yeyote atakayekutwa hana kitambulisho hataruhusiwa kufanya biashara na hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake,” amesema Makonda.

Amewataka wafanyabiashara wenye sifa za kupata vitambulisho  kufika ofisi za wilaya na serikali za mitaa kufuata utaratibu wa kuvipata.