Mbunge wa Chadema akamatwa akitoka bungeni

Muktasari:

 Polisi mkoani Dodoma wanadaiwa kumkamata mbunge wa Mbozi (Chadema) leo jioni Jumatatu kwa tuhuma ambazo hazijafahamika

Dodoma. Mbunge wa Mbozi (Chadema) Pascal Haonga amekamatwa na polisi jioni wakati akitoka katika kikao cha Bunge leo jioni Jumatatu Mei 6, 2019 jijini Dodoma.
Akizungumza na Mwananchi, Mbunge wa Momba (Chadema) David Silinde amesema hawajajua sababu ya kukamatwa kwake mbali ya kuambiwa kosa lake limefunguliwa jalada mkoani Songwe.
"Ni kweli amekamatwa nje ya geti wakati akitoka bungeni leo jioni. Hajaambiwa kosa na wala sisi hatujui kosa. Tuko kwa RCO ( Mkuu wa Upelelezi)  wanasema wanasubiri gari la kumpeleka Songwe," amesema.
Alipoulizwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema hana taarifa za kukamatwa kwa mbunge huyo.
"Niko Gairo sijapata taarifa zozote za  kukamatwa kwa mbunge huyo," amesema Muroto.

Soma: