Mwinyi akerwa na michango ya wabunge ya kulibeza jeshi

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Hussein Mwinyi akisoma hotuba ya kambi rasmi ya upinzani katika Wizara yake ambayo imewasilishwa bungeni jijini Dodoma leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

  • Waziri wa Ulinzi, Dk Hussen Mwinyi amekemea siasa katika vyombo vya ulinzi akisema jeshi linatimiza wajibu wake.

Dodoma. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussen Mwinyi ameliambia Bunge leo Alhamisi Mei 16,2019 kuwa katika mambo ya ulinzi watu wasiingize siasa.

Dk Mwinyi amesema kuwa michango ya baadhi ya wabunge iliyotolewa leo bungeni imemsikitisha sana kwa sababu anajua siku zote wabunge hufanya kazi ya kuunga mkono, lakini tofauti na leo.

Amesema jeshi limekuwa likifanya kazi kwa weledi mkubwa katika kila eneo wanalopangiwa hivyo hakuna sababu ya kuwabeza.

“Tuangalie nchi za wenzetu huko, sasa mkiona kwetu pametulia mjue siyo bure, kuna kazi imefanyika na hawa tunaowabeza,” amesema Dk Mwinyi.

Kuhusu JWTZ kushutumiwa kwamba wanaingilia kazi za vikosi vingine vya ulinzi, amesema siyo kosa kwa sababu kazi ya ulinzi inahusisha vikosi vyote.

Amesema mkuu wa majeshi ndiye mwenyekiti wa vyombo vya ulinzi nchini, hivyo anayo haki ya kuvisemea vyombo vingine katika ulinzi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mwinyi amesema maslahi ya wanajeshi yamekuwa yakiboreshwa mara kwa mara lakini katika kipindi cha 2015/16 hadi sasa wameshaboreshewa kwa asilimia 15.