Sheikh wa Mkoa Dar agusia ya Spika Ndugai, CAG

Sheikh wa mkoa wa Dar es Salaam,  Alhad Mussa Salum 

Muktasari:

Rais wa Tanzania, John Magufuli leo Ijumaa ameshuhudia makabidhiano ya mfumo wa usimamizi wa mawasiliano ya simu kati ya TCRA na kampuni ya SGS jijini Dar es Salaam


Dar es Salaam. Sheikh wa mkoa wa Dar es Salaam,  Alhad Mussa Salum amempongeza Spika wa Bunge, Job Ndugai akisema ni kiongozi ambaye akimuita mtu lazima aende.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Januari 18, 2019 wakati akisoma dua katika hafla ya makabidhiano ya mfumo wa kusimamia uwazi katika mawasiliano ya simu (TTMS) iliyofanyika katika Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) jijini Dar es Salaam.

Amewataka Watanzania kuendelea kuwaombea viongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano akiwemo Ndugai kwa kusimamia haki ndani ya mhimili anaouongoza.

“Tunaendelea kumuombea uhifadhi na kumlinda Rais wetu yeye na Makamu wa Rais, Waziri Mkuu pamoja na Spika wetu ambaye unaendelea kumpa afya, ambaye akimwita mtu ni lazima aende, ni jambo jema kwa sababu ni mhimili wa kutosha. Tunaendelea kumuombea kwa jambo jema hilo,” amesema Sheikh Alhad.

Licha ya kutotaja Ndugai amemuita kiongozi gani, lakini jana Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad alieleza nia yake ya kufika mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge Januari 21, 2019 ikiwa ni agizo la Ndugai baada ya CAG kudaiw akutoa kauli za kulidhalilisha Bunge.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, siasa wakiongozwa na Rais wa Tanzania, John Magufuli.

Kiongozi huyo wa kiroho amesema Serikali imewapa mamlaka viongozi wa dini kuliko awamu yoyote huku akimuomba Mungu aendelee kuwapa afya na maisha marefu viongozi.