Tanzania yawakaribisha wawekezaji wa korosho

Baadhi ya washiriki wa kongamano la kimataifa la uwekezaji katika sekta ya ubanguaji wa korosho lililoandaliwa na kituo cha uwekezaji nchini (TIC) Picha na Haika Kimaro

Muktasari:

Katika kuhakikisha korosho inabanguliwa nchini Tanzania Kituo cha Uwekezaji (TIC) kimeandaa kongamano la korosho la kimataifa linalolenga kuvutia wawekezaji.

Mtwara. Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi amesema mkoa huo  umetenga eneo la zaidi ya ekari 2,000 kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vya korosho.

Amesema eneo hilo ni kwa wawekezaji watakaovutiwa kuwekeza mkoani humo.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Julai 12, 2019 katika kongamano la kimataifa la uwekezaji katika sekta ya ubanguaji wa korosho lililoandaliwa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) linalofanyika mkoani Mtwara na kujumuisha kutoka nchi 10.

Zambi amesema wamedhamiria kuongeza uzalishaji wa korosho na wanawaalika  wawekezaji kuwekeza katika viwanda ili kulinda ajira na bidhaa nyingine zinazotokana na korosho kuzalishwa  nchini.

Amewahakikishia amani na usalama nchini na watakaoweza wawe na uhakika mali watakazowekeza hazitapotea.

Amesema mkoa huo ulikuwa ukizalisha korosho kwa kiasi kidogo lakini kwa miaka miwili uzalishaji ulianza kuongezeka kutokana na jitihada za serikali wanatenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji na ndani ya miaka mitatu wameweza kusambaza miche mipya ya korosho zaidi ya milioni 7.

“Mwaka 2015/16 tulianza na tani 28,000, mwaka 2016/17 tulizalisha tani 61,000  na mwaka 2017/18 tani 76,000 na mwaka huu kwa sababu ya hali ya hewa haikuwa nzuri sana tulizalisha tani 56,000 lakini pia tumeendelea kuongeza vitalu kwa ajili ya uzalishaji,” amesema Zambi.