Treni yapata ajali, mabehewa ya mahindi na ngano yaanguka

Muktasari:

Treni ya mizigo iliyokuwa ikitokea mkoani Tabora kuelekea Mwanza imepata ajali na mabehewa kadhaa yaliyokuwa na ngano na mahindi yameanguka


Kwimba. Treni ya mizigo iliyokuwa ikitokea mkoani Tabora kuelekea Mwanza imepata ajali na mabehewa kadhaa yaliyokuwa na ngano na mahindi yameanguka.

Ajali hiyo imetolea leo Alhamisi Julai 18, 2019 katika kijiji cha Kitunga wilayani Kwimba Mkoa wa Mwanza.

Akizungumza na Mwananchi Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo, kwamba usalama umeimarishwa na mizigo ipo salama.

"Ni kweli taarifa ninazo mabehewa machache ya mahindi na ngano yameanguka Kwimba, ni ajali ya kawaida bado chanzo hakijajulikana," amesema kamanda Muliro

Mkuu wa Wilaya ya Kwimba, Senyi Nganga alipoulizwa na Mwananchi kuhusu ajali hiyo amesema alikuwa katika gari akielekea eneo la tukio.

Mmoja wa mashuhuda wa ajali hiyo, Richard Lutobeka amesema mabehewa yaliyoanguka ni saba kati ya 24 na kwamba ajali hiyo ilitokea saa 8:45 mchana.