Waziri Mkuu ashangazwa viongozi Kilimanjaro kuchapana makonde ofisini

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa

Muktasari:

 

  • Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema tabia zinazoendelea kwa baadhi ya viongozi wa mkoa wa Kilimanjaro zinalitia aibu Taifa huku akiwashangaa kutofuata maelekezo ya mkuu wa mkoa.

Dodoma. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema tabia zinazoendelea kwa baadhi ya viongozi  wa mkoani Kilimanjaro zinalitia aibu Taifa na kuwashushia hadhi wahusika.

Majaliwa ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Januari 26, 2019 mkoani Dodoma wakati akifungua mkutano wa siku moja kwa wakuu wa mikoa unaolenga kujadili namna bora ya upatikanaji wa masoko ya madini nchini.

Amesema taarifa alizozipata kutoka Kilimanjaro kwamba viongozi walipigana ofisini na kubainisha kuwa hilo si jambo zuri huku akishangazwa na watu hao kushindwa kufuata maelekezo ya mkuu wa mkoa.

“Hivi kuna nini Kilimanjaro, eti mkuu wa mkoa tueleze, inakuwaje hivi karibuni tunaleta mawaziri wakazungumza kwa mapana na tukadhani kumetulia lakini ghafla tena watu wanapigana ngumi, hii ni aibu, "amesema Majaliwa.

“Hatupendi kufika huko lakini msitulazimishe na mamlaka husika ziamue kuchukua hatua, si jambo jema, lazima mambo kama haya yasipewe nafasi kabisa.”

Amesema lengo la uteuzi kwa viongozi ni kutakiwa kufanya mambo ambayo kiongozi wao anayafanya ikiwemo kushirikiana na viongozi na taasisi nyingine na kukaa pamoja na kujadiliana kuhusu rasilimali za nchi.