East Africa’s Got Talent kuchimba mgodi wa vipaji Afrika Mashariki

Mashindano ya America’s Got Talent, Britain’s Got Talent ni maarufu sana duniani kote. Sasa mashindano haya yamekuja Afrika Mashariki kusaka vipaji vya kila aina.

Tofauti na Pop Idol, BSS au Project Fame, mashindano haya yatachukua vipaji vya aina zote.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo kwa utani alisema hata wale wenye uwezo wa kuzuia mvua wanakaribishwa kushiriki.

Takribani siku tatu zilizopita mashindano hayo yatakuwa chini ya usimamizi wa Clouds Media International, yalizinduliwa ikiwa ni siku moja baada ya Kenya.

Mchekeshaji wa Uganda, Anne Kansiime atakuwa mtangazaji katika mashindano hayo yatakayochukua vipaji kutoka nchi za Kenya, Uganda, Tanzania na Rwanda.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mashindano hayo, Mkurugenzi wa Clouds Media Group, Joseph Kusaga amesema haikuwa rahisi kupata kibali cha kuyaendesha kutokana na vigezo vingi vya ubora kuhitajika.

“Tumefurahi kufanikisha kuyaleta mashindano haya Afrika Mashariki, tunaamini yatatoa nafasi kwa watu wenye vipaji, pia, kuwapa jukwaa la kuionyesha dunia kilichopo katika ukanda huu,” amesema.

Kusaga ameongeza kuwa: “Hili si shindano la kupata zawadi bali la kuonyesha kila mmoja alichonacho. Ukionyesha kipaji kinaweza kubadili kabisa maisha yako.”

Shoo hiyo itakayorushwa katika vituo mbalimbali vya televisheni itatayarishwa na Kampuni ya Rapid Blue ambayo pia ndio wanaotayarisha katika nchi za Afrika Kusini na Nigeria.

Kila nchi kutoa jaji mmoja

Mashindano hayo yataendeshwa na majaji kama inavyofanyika katika nchi nyingine takribani 58.

Kwa upande wake Dk Mwakyembe, amesema atahakikisha anahamasisha mshindi wa East Africa’s Got Talent’ anatoka Tanzania na kulamba zawadi ya Sh120 milioni ya zawadi.

Amesema mashindano hayo ni makubwa na yanatambulika duniani hivyo kuna kila sababu ya Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki ukizingatia litajumuisha vipaji mbalimbalimbali.

Aidha amesema watalitumia shindano hilo katika kutangaza utalii kwani pamoja na kuwa nchi yenye mbuga za hifadhi nyingi ukilinganisha na nyingine za Afrika Mashariki, bado tupo nyuma katika uingizaji wa watalii.

Anne Kansiime ambaye ni mchekeshaji maarufu kutoka nchini Uganda, amesema amefurahi kuchaguliwa kuwa mmoja wa majaji na kueleza watu wa Afrika Mashariki wana kila sababu ya kulitumia ili kuzalisha wasanii wengine wapya.

“Tunahitaji wakina Kansiime wengi. Wakina Diamond wengine kwani na sisi itafika mahali kazi hii tutaacha,” amesema Kansiime.