ANTI BETTIE: Tatizo ni kwamba ananiaibisha kila mara nikiwa naye faragha

Anti habari yako!

Niokoe nakaribia kuachana na mpenzi wangu kutokana na namna anavyopiga mayowe tukiwa faragha.

Nashindwa nifanyeje, maana haelewi.

Kiasi nimecheka. Anapiga yowe tena siyo anaugulia kwa mahaba, au unamuumiza?

Kuugulia, kuzungumza zungumza namna unavyojisikia wakati wa faragha ni jambo zuri na linaamsha mshawasha wa kuendelea na mlilokusudia, ila hili la huyu mpenzi wako ndiyo jipya.

Anza na mbinu ya kawaida, baada ya vurugu zote ukiona amekolea na anakaribia kuanza mayowe mpe ‘denda’ na ufanye hivyo muda wote hadi mtakapoamua kuahirisha.

Fanya hivi bila kuacha na mara zote mnapokuwa faragha, anaweza kujaribu kukutoa usikubali kwa sababu lengo ni kudhibiti mayowe yake.

Mkiahirisha shughuli hiyo mweleze kuwa utafanya hivyo mara zote hadi atakapopunguza mayowe na kuugulia kimahaba.

Kingine, punguza majonjo, inawezekana ni miongoni mwa wanawake wanaokolewa sana na hayo mambo, hivyo nenda naye taratibu ukiona amekolea unapunguza dozi hatua kwa hatua. Ila jambo zuri ni kuendelea kumsisitiza kuwa umechoka fedheha zake na namna zinavyohatarisha uhusiano wenu.

Kwa kuwa hujafunga naye ndoa inawezekana anazidisha heka heka kukuhamasisha umuoe, unaonaje ukianza mikakati ya ndoa kuliko kuruhusu uhawara sugu.

Sitaki kuzaa naye familia yake haijielewi

Nimeolewa huu mwaka wa tatu, ninampenda mume wangu lakini sitaki kuzaa naye kutokana na tabia za familia yake, walevi, waongo na wezi, nahisi nitaanzisha kizazi kitakachopata taabu.

Nifanyeje?

Waswahili waliwahi kusema ‘Ukilipenda boga...penda na ua lake’, hivyo kama umempenda kweli mumeo huna budi kuwapenda na kuwaheshimu ndugu zake.

Halafu umeolewa na familia, hao watoto unaizalia familia au unajizalia wewe na mumeo? Kuwa na adabu, acha kudhihaki familia za watu, mpaka umefunga naye ndoa bila shaka uliridhika na tabia zake na familia yake, hayo unayoyaleta sasa ni dharau na utovu wa nidhamu wa hali ya juu.

Zungumza haya maneno uliyoyaandika kwa nguvu halafu ujisikilize wewe mwenyewe kama unachokisema ni sahihi au unapotoka?

Tuliza akili linda ndoa yako na inawezekana wewe ndiyo ukawa chanzo cha kuwabadili hao unaowaita wezi, walevi na waongo.

Muombe Mungu pia akupe kizazi chema, unaweza kukataa kuzaa na familia hiyo ukaenda kuzaa kwa wenye maadili, lakini uzao wako ukawa chanzo cha laana kwenye familia hiyo.

Xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Eti! Nikimsomesha mwanamke atanikimbia?

Kuna binti tumependana na nimempenda zaidi kutokama na jinsi anavyopenda kujiendeleza kielimu, miongoni mwa makubaliano yetu ni pamoja na kumsomesha ngazi ya stashahada. Rafiki zangu wananitisha kuwa mwanamke hasomeshwi na nikifanya hivyo kabla ya ndoa ua baada atanikimbia.

Nifanyeje?

Unachotakiwa kuangalia ni namna mlivyopendana na uaminifu wa kila mmoja kwa mwenzake.

Kumsomesha au kutofanya hivyo siyo kipimo cha mapenzi, kama utamsomesha iwe kwa mapenzi yako na si makubaliano au lazima.

Kuhusu hao rafiki zako wanaosema mwanamke hasomeshwi hawapo sahihi kwa sababu wapo wanawake waliwasomesha wanaume na waliwaacha solemba.

Hivyo suala la usaliti baada ya kufanyiwa kitu fulani siyo la wanawake peke yao, hata wanaume wapo wanaofanya hivyo. Haimaanishi mkisomeshana hata mkishindwana tabia mng’ang’aniane .

Nakukumbusha penzi imara ni la mtu na mpenzi wake, likiingiza marafiki ni igizo na siyo uhusiano tena.