Odinga atuma salamu za rambirambi ajali ya MV Nyerere
Muktasari:
Kiongozi wa muungano wa upinzani wa Nasa, Raila Odinga amekuwa kiongozi kwa kwanza nje ya nchi kutuma salamu za rambirambi kufuatia kivuko cha MV Nyerere kuzama mkoani Mwanza
Dar es Salaam. Kiongozi wa muungano wa upinzani wa Nasa nchini Kenya, Raila Odinga amekuwa kiongozi kwa kwanza nje ya nchi kutuma salamu za rambirambi kufuatia kivuko cha MV Nyerere kuzama mkoani Mwanza.
Kivuko hicho kilizama jana mchana Septemba 20, 2018 na hadi leo asubuhi Septemba 21, 2018 maiti za watu 86 zimeopolewa.
Katika ujumbe wake alioutuma katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter, Odinga ametoa pole kwa Watanzania kufuatia ajali hiyo.
“ Naomboleza pamoja na raia wa Tanzania katika kipindi hiki kigumu. Mungu awape amani na nguvu familia, watoa faraja na Taifa la Tanzania,” amesema.
Jana, Rais John Magufuli alituma salamu za rambirambi na kuelezea masikitiko yake kufuatia ajali hiyo.