VIDEO-Ajali iliyotokea Uganda yasababisha vifo vya Watanzania 13

Muktasari:

  • Taarifa kutoka Uganda zinaeleza kwamba Watanzania 13 waliokuwa kwenye basi hilo wamefariki na wengine wanane kujeruhiwa vibaya baada ya basi hilo kugongwa na lori.

 Kamanda wa Polisi mkoa wa Kagera, Augustine Ollomi amethibitisha taarifa ya ajali ya gari iliyotokea Uganda na kuhusisha basi aina ya Costa lenye namba za Tanzania na lori la Uganda ambalo lilikuwa limetokea Dar es Salaam.

Taarifa kutoka Uganda zinaeleza kwamba Watanzania 13 waliokuwa kwenye basi hilo wamefariki na wengine wanane kujeruhiwa vibaya baada ya basi hilo kugongwa na lori.

Kamanda Ollomi amesema Watanzania hao walikwenda Uganda kwa ajili ya shughuli ya harusi lakini hana taarifa walikwenda sehemu gani nchini humo. Amesema wanaendelea kufanya mawasiliano na mamlaka za Uganda kujua undani wa ajali hiyo.

“Ni kweli tumefuatilia basi hilo na kubaini kwamba liliondoka hapa nchini Septemba 15 kwenda Uganda kwenye shughuli ya harusi. Mengine siwezi kusema zaidi mpaka tutakapofanya mawasiliano na mamlaka za Uganda,” amesema Ollomi.

Gazeti la Uganda la Daily Monitor limeandika mtandaoni kwamba Watanzania hao walikwenda Uganda kwenye harusi ya binti yao, Dk Annette Ibingira ambaye amefunga ndoa na Mganda, Dk Treasurer Ibingira.

Majeruhi walipelekwa Hospitali ya Nkozi kwa ajili ya matibabu lakini baadaye walipewa rufaa na kupelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mulago. Maiti zote zilipelekwa Hospitali ya Gombe.