Polisi Iraq yaua waandamanaji

Muktasari:

Wakati hayo yakijiri Baraza la Mawaziri la Iraq linatarajia kuwa na kikao cha dharura kujadili hatua ya kujiuzulu kwa Waziri Mkuu, Adel Abdul Mahdi pamoja na maafisa wengine waandamizi wa Serikali.

Baghdad, Iraq. Vikosi vya usalama nchini Iraq vimewafyatulia risasi za moto na kuwaua waandamanaji wawili na kujeruhi wengine 26.

Waaandamanaji hao wameuawa jana Jumamosi Novemba 30 katika mji miwili ya Najaf na Baghdad.

Tukio hilo katika kipindi ambacho machafuko yanayoendelea katika nchi hiyo kufuatia muda mchache baada ya Waziri Mkuu, Adel Abdul-Mahdi kutangaza nia yake ya kujiuzulu.

Taarifa ya Jeshi la Polisi nchi Iraq zilisema kuwa vifo hivyo vimetokea baada ya vikosi vya usalama kufyatua risasi za moto dhidi ya waandamanaji katika mji mtakatifu wa Najaf, Kusini mwa Iraq pamoja na mji mkuu wa Baghdad.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa watu 11 wamejeruhiwa katika daraja la Ahrar mjini Baghdad wakati vikosi vya usalama vilipowafyatulia risasi kuwarushia mabomu ya machozi ili kutawanya waandamanaji hao.

Katika hatua nyingine, Baraza la Mawaziri la Iraq limeitisha kikao cha dharura kujadili hatua ya kujiuzulu Kwa waziri mkuu wa nchi hiyo pamoja na maafisa wengine waandamizi wa Serikali.

Jumamosi iliyopita Waziri Mkuu, Adel Abdul Mahdi alitangaza azma yake ya kuwasilisha kwa Bunge barua ya kujiuzulu wadhifa huo.

Uamuzi huo wa Mahdi umeafikiwa baada ya umwagaji wa damu ya waandamanaji wanaoipinga Serikali ya Iraq kwa vitendo vya rushwa, ukosefu wa ajira na kudorora kwa huduma za jamii.