Kinana, Makamba sasa shubiri CCM

Dar es Salaam. Makatibu wakuu wa zamani wa CCM, Abdulrahman Kinana na Yusuf Makamba sasa wamekuwa chungu ndani ya chama hicho baada ya kutoonekana mbele ya Kamati ya Maadili kuhojiwa, huku kukiwa na ubashiri kuwa wamekiachia chama hicho mamlaka ya kuamua hatima yao.

Kinana, Makamba na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bernard Membe waliitwa mbele ya kamati hiyo baada ya sauti zao kuenea katika mitandao ya kijamii zikieleza jinsi CCM inavyopoteza mvuto, uendeshaji nchi na jinsi chama kilivyoshindwa kuwalinda makatibu huo dhidi ya mtu anayewachafua.

Membe alifika mbele ya kamati hiyo yenye wajumbe wanne Jumanne na baada ya hapo alieleza kufurahishwa na mazungumzo, akisema Mungu alimpa ujasiri wa kuzungumza kile alichotaka kuiambia kamati hiyo na kwamba hakuyumba wala kuyumbishwa katika mahojiano.

Wengine ambao sauti zao zilisikika katika mkanda huo ni Nape Nnauye, ambaye ni mbunge wa Mtama, William Ngeleja (Sengerema) na January Makamba (Bumbuli) walimuomba radhi Rais John Magufuli.

Kwa mujibu wa mwenyekiti wa kamati hiyo, Phillip Mangula akinukuliwa na gazeti la chama hicho, baada ya Membe, wangehojiwa makatibu hao ndani ya wiki iliyoisha, lakini hilo halikuwezekana juzi na jana baada ya wajumbe wa kamati hiyo kumsubiri Kinana hadi jioni ya Ijumaa bila ya mafanikio.

Kuna habari nyingine kuwa Makamba na Kinana wanaweza kuhojiwa kesho jijini Dodoma au Dar es Salaam, huku ikielezwa kuwa kikao cha Kamati Kuu ya CCM ambacho kingefanyika kesho, kimesogezwa mbele kwa siku moja.

Habari zilizozagaa ni za wawili hao kujivua uanachama kuepuka adhabu inayoweza kuwadhalilisha kama watendaji wakuu wa zamani wa chama hicho, iwapo kamati hiyo itawaona na hatia na baadaye kutangaza kuwavua uanachama au kuwachukulia hatua nyingine, kama kuwapa onyo.

Iwapo hawatajitokeza mbele ya kamati hiyo, CCM itakuwa katika wakati mgumu wa kuamua mustakabali wa watu walioshika nafasi nyeti ya utendaji mkuu baada ya kuondoka kwa mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye kukisumbua chama hicho katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Lowassa, ambaye alikwazika na kutopitishwa kugombea urais, aliondoka na kundi la watu, wakiwemo mawaziri, wabunge, wenyeviti wa mikoa, madiwani na wanachama, huku baadhi ya waliosalia wakikisaliti chama katika uchaguzi mkuu.

Lakini kwa mujibu wa wachangiaji katika mijadala hiyo, juhudi zinaendelea kuwahakikishia makatibu hao kuwa hawatachukuliwa hatua za kuwadhalilisha na hivyo kuwashauri kutokea mbele ya kamati ili kumaliza tatizo lao.

Jana kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete mjini Dodoma, ambako kulikuwa na kongamano la CCM, hotuba ya Mangula ilijikita katika uchaguzi mkuu ujao, hakugusia kabisa suala la makatibu hao.

Alipomaliza, aliruhusu maswali kutoka kwa wanachama na sehemu hiyo iliongozwa na mwenyekiti wa CCM mkoa. Alipomaliza, alitokea mlango uliopo karibu na jukwaa na juhudi za waandishi kumsogelea ili kumuuliza maswali kuhusu sakata hilo, hazikufanikiwa.

Kutoonekana kwa Kinana Ijumaa kumeacha sintofahamu si tu kwa wananchi ambao wanafuatilia suala hilo, jana baadhi waliamua kuhamishia hisia zao katika mitandao ya kijamii.

“Wawaachie lichama lao, waache kusumbua wazee wa watu na makamati yao ya maadili,” ameandika mtu aliyejiita Dk Lema akichangia mjadala katika akaunti ya Twitter iliyoweka taarifa inayoeleza kuwa makatibu hao wamejiuzulu uanachama wa CCM.

Mwingine anayejiita M.A. Aubameyang aliandika katika mjadala mwingine akisema: “Acha unafiki ww, nyie ndio mlikuwa wa kwanza kumsema Kinana, leo unamtetea na chama ni cha watu si mtu.”

Makamba na Kinana waliingia katika mgogoro na uongozi baada ya kuandika barua ya kuulalamikia kuwa hauwalindi dhidi ya mtu anayejiita mwanaharakati wa Serikali ya Awamu ya Tano, wakidai anawachafua lakini kutokana na kulindwa na “mtu mwenye mamlaka”, amekuwa akiendelea kuwadhalilisha.

Makamba hajaonekana kuwa na mgogoro na uongozi kabla ya barua hiyo, lakini hata kabla ya kuondoka ofisini, Kinana alikuwa haonekani katika mikutano kadhaa ya vikao vya juu na wakati fulani ilibidi mwenyekiti wake, John Magufuli azime uvumi kuwa amejiuzulu, aliposema kuwa amemruhusu kwenda India kwa matibabu.

Mbali na Mangula, wajumbe wengine wa kamati hiyo ni katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ali, mjumbe wa Kamati Kuu, Hassan Juma na mjumbe mmoja ambaye Mwananchi ilishindwa kupata jina lake.