VIDEO: Alichosema Dk Mashinji baada ya Mdee kukataa salamu yake

Muktasari:

Akizungumza na Mwananchi leo Februari 25, 2020 aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Mashinji amesema kuwa atamsalimia Halima Mdee atakapokutana naye

Dar es Salaam. Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Vicent Mashinji amesema kitendo cha Mbunge wa Kawe, Halima Mdee kugoma kumpa mkono sio cha kistaarabu.

Tukio hilo lilitokea jana Jumanne Februari 24, 2020 nje ya Mahakama ya Kisutu ambapo viongozi wa Chadema walifika kusikiliza kesi yao ya uchochezi inayowakabili na Dk Mashinji alianza kuwasilimia wengine lakini alipompa mkono Mdee kwa ishara ya salamu aligoma.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu ilipotaka kujua anazungumziaje tukio hilo Dk Mashinji amesema kitendo hicho sio ustaarabu na kwa mila na desturi za Afrika hicho kitu huwa hakipo.

“Binafsi ninaamini alikuwa na shida fulani, huwezi jua mtu kaamkaje na alikuwa anawaza nini labda yeye anaweza akaeleza vizuri,” amesema Dk Mashinji

Dk Mashinji alihamia CCM, Februari 18, 2020 amesema suala hilo halitamzuia kumsalimia pindi wakikutana tena mahala popote.

Mdee alipohojiwa kuhusu kitendo alichokifanya alisema “achana naye ni mnafiki…”