Basi lapinduka Kilimanjaro, 40 wanusurika

Muktasari:

Abiria zaidi ya 40 wamenusurika kifo baada ya basi la Kaprikon walilokuwa wamepanda kupinduka karibu na eneo la KIA wilayani Hai, mkoani Kilimanjaro nchini Tanzania.

Hai. Watu zaidi ya 40 wamenusurika kifo baada ya basi la kampuni ya Kaprikon walilokuwa wanasafiria kutoka Singida kwenda Moshi mkoani Kilimanjaro  nchini Tanzania kupata ajali na kupinduka eneo la KIA wilaya ya Hai Mkoa wa Kilimanjaro.

Akizungumza na Mwananchi, George Benedict Mberessero ambaye ni mmiliki  wa mabasi hayo amesema ajali hiyo imetokea leo Jumanne Agosti 13,2019.

Amesema ajali hiyo imetokea saa 10  jioni baada ya basi hilo kulipisha gari lililobeba  fedha ambalo lililokuwa likitoka jijini Dar es Salaam kwenda mkoani Arusha.

"Ni kweli gari limepata ajali maeneo ya KIA likitokea mkoani Singida kuja Moshi na kwamba chanzo cha kupinduka kwa basi hilo inatokana na kupisha gari... lililobeba fedha ndipo lilipoanguka,” amesema Mberessero

"Hakuna madhara yoyote  yaliyojitokeza kwani basi lilikuwa kwenye mwendo wa taratibu," amesema

Jitihada za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro zinaendelea