Dk Bashiru: Nilitamani kujiuzulu ukatibu mkuu CCM

Muktasari:

Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema kuna wakati alitaka kujiuzulu wadhifa huo lakini alipewa moyo na Rais John Magufuli na watu wake wa karibu, kubainisha kuwa mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na wa Mbeya, Albert Chalamila watakuwa viongozi vijana wa kwanza kusoma somo la uongozi


Dar es Salaam. Katibu mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania, Dk Bashiru Ally amesema wadhifa alionao ulikuwa mzigo kwake na ilifikia wakati alitaka kujiuzulu lakini alipewa moyo na mwenyekiti wa chama hicho, Rais John Magufuli na watu wake wa karibu.

Dk Bashiru ametoa kauli hiyo leo Jumatano Agosti 28, 2019 katika Shule ya Msingi Ubungo Kisiwani katika siku ya pili ya ziara yake jimbo la Ubungo.

“Siasa za kiutendaji na usimamizi wa chama kikubwa kama hiki nina umri wa mwaka mmoja, nilikejeliwa sana nikaitwa majina ya uonevu wakati mwingine nampigia mwenyekiti (Magufuli)  hii kazi uliyonipa vipi.”

“Mtoto wangu mkubwa alisema kama angekuwa na hiari kuamua kazi inayonifaa angeniambia baba achana na kazi hii (ya ukatibu mkuu), Magufuli alinishauri maana anajua misukosuko ya uongozi,” amesema Dk Bashiru.

Pia, aliwataja mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na wa Mbeya, Albert Chalamila kwamba wanatakiwa kurejea shule kusoma somo la uongozi.