Dk Makongoro Mahanga afariki dunia

Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Ilala, Dk Milton Makongoro

Muktasari:

Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Ilala nchini Tanzania, Dk Milton Makongoro Mahanga ambaye pia alishawahi kuwa Naibu Waziri wa Kazi na Ajira amefariki dunia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) alikokuwa akipatiwa matibabu.

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Ilala, Dk Milton Makongoro Mahanga amefariki dunia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) alikokuwa akipatiwa matibabu.
Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu leo Jumatatu Machi 23, 2020 Katibu wa Chadema Kanda ya Pwani, Hemed Ally amesema wamepata taarifa za msiba huo.
“Ni kweli taarifa hizo tumezipata kupitia katibu wa Chadema wa Mkoa wa Ilala maana yeye ndiye alikuwa anafanya naye kazi kwa ukaribu,” amesema.
Ally amesema leo Jumatatu walikuwa wamepanga kwenda Muhimbili kumuona lakini kabla hawajaenda walipata taarifa kuwa ameshafariki dunia.
“Ilikuwa twende tukamuone leo na taarifa zote zilikuwa zinapitia kwa katibu wake wa mkoa wa Ilala wa chama, sasa asubuhi alipofanya mawasiliano na mke wake akamueleza kuwa Dk Makongoro amefariki,” amesema.