Erick Omondi, Mc Pilipili ‘kuwavunja mbavu’ wakazi wa Dodoma

Muktasari:

  • Wasanii Mc Pilipili na mchekeshaji kutoka nchini Kenya, Erick Omondi wanatarajia kupanda jukwaa moja kuwachekesha wakazi wa mji wa  Dodoma na viunga vyake huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Naibu Waziri Anthony Mavunde.

Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu nchini Tanzania, Anthony Mavunde anatarajia kuwa miongoni mwa wakazi wa Jiji la Dodoma watakaoshuhudia shoo ya wachekeshaji Emmanuel Mathias maarufu Mc Pilipili na mchekeshaji kutoka nchini Kenya, Erick Omondi.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu  Septemba 9,2019 Pilipili amesema shoo hiyo itafanyika Septemba 28,2019 jijini Dodoma nchini Tanzania.

Hii itakuwa mara ya kwanza kwa Omondi kupanda jukwaa moja Pilipili.

Akielezea shoo hiyo, Mc Pilipili amesema Omondi kwa muda mrefu amekuwa akimvutia na hii ni tangu alipoanza kazi ya uchekeshaji na kuongeza kuwa ni moja ya watu waliomvutia kuingia katika fani hiyo.

“Omondi ndiye aliyenifanya niingie kwenye sanaa ya uchekeshaji kwani ni msanii ambaye ninakubali kipaji chake na huenda kama sio yeye labda mimi ningekuwa nafanya kazi ya ushehereshaji tu,” amesema  Mc Pilipili.

Amefafanua kubwa onyesho hilo litasindikizwa na wasanii wa vichekesho wakiwamo  Dullyvani, Dogo Pepe, Ally na Oscar Nyerere na bendi ya bendo TNC kutoka mkoani Dodoma.

Amesema mgeni rasmi atakuwa Mavunde ambaye pia ni Mbunge wa Dodoma Mjini (CCM) pamoja na wabunge na mawaziri.