Kampeni kuwahamasisha wananchi kutunza fedha benki yazinduliwa

Muktasari:

  • Benki ya NBC imezindua kampeni ya kuhamasisha Watanzania kutunza akiba zao benki, Mpango huo huenda ukaongeza kiasi cha amana katika benki hiyo lakini pia kinaongeza nguvu katika mkakati wa nchi wa kujumuisha watu wengi katika huduma za kifedha.

Dar es Salaam. Benki ya NBC imezindua kampeni ya miezi sita kwa lengo kuhamasisha wananchi kutunza akiba huku ikitoa ofa na zawadi mbalimbali kwa watakaoibuka washindi katika kipindi hicho.

Miongoni mwa zawadi zitakazotolewa wakati wa kampeni hiyo ni fedha taslimu, pikipiki za magurudumu mawili 20 na za magurudumu matatu pamoja na safari ya kitalii kwa watu 16 kati yao sita wakipelekwa katika mbuga za Serengeti na wengine 10 visiwa vya Ushelisheli.

Kampeni hiyo ilizinduliwa jana Jumatatu Septemba 30, 2019 na inatarajiwa kuwafikia maelfu ya Watanzania hususani wale ambao bado hawajafikiwa na huduma za kibenki, watahamasishwa kuweka akiba kupitia akaunti ya Malengo.

Akizungumza wakati hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo, Kaimu Mkurugenzi wateja wa Rejareja wa Benki ya NBC, Benjamin Nkaka alisema kampeni hiyo inalenga kuleta mabadiliko kwenye mtazamo wa uhifadhi wa akiba miongoni wa wananchi kutoka kuhifadhi pesa majumbani na badala yake wazihifadhi kupitia benki hiyo huku wakifurahia faida.

“Ni wakati muafaka sasa kwa Watanzania kuacha kuhifadhi fedha zao kwenye vibubu au namna nyingine yoyote ambayo si salama kwao na kiuchumi kwani wanaweza kuhifadhi pesa zao kupitia akaunti ya Malengo ya NBC. Habari njema zaidi ni kwamba hakutakuwa na makato ya mwezi bali mteja atapata riba ya hadi asilimia saba kwa mwezi,’’ alisema Nkaka.

Aidha Nkaka alisema kampeni hiyo, inawalenga wateja wote wapya na ambao tayari wanamiliki Akaunti ya aina hiyo na watakaoshinda ni mtu mmoja sio taasisi wala kampuni.