Magufuli aomba orodha mawaziri, wakurugenzi na makatibu wakuu wenye laini za TTCL

Rais John Magufuli

Muktasari:

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba ameagizwa kuandaa orodha ya namba za makatibu wakuu, wakurugenzi na mawaziri wanaotumia namba za TTCL.

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amemuagiza mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba kumuorodheshea namba za makatibu wakuu,  wakurugenzi na mawaziri wanaotumia mtandao wa simu wa TTCL.

Magufuli ametoa kauli hiyo leo Jumanne Mei 21, 2019 jijini Dar es Salaam katika hafla fupi ya shirika hilo kukabidhi gawio lake serikalini.

Amebainisha kuwa mwezi mmoja tangu kufanya hivyo wataangalia viongozi wa Serikali wanaolipwa mshahara na hawana namba za TTCL.

“Na zisiwe zimekatwa tu, ziwe zinatumika  asije kuwa anaandika tu meseji halafu anaifunga. Na wewe ( Kindamba)  ufanye hivyo kwa wafanyakazi wako kwa sababu kama unao wafanyakazi 1,500 unaweza kukuta hawafiki hata 100 wenye laini za TTCL.”

“Ombi kubwa kwa Watanzania, ni lazima tujali vitu vyetu, niwaombe viongozi wa dini, najua mnatuombea sana tusifanye dhambi na tuzishike amri lakini mtuombee pia tutambue wajibu wa kuvithamini vyetu ikiwemo TTCL,” amesema Magufuli.