Makonda ataka kukutanishwa na ‘wanaokesha’ wakibishana mitandaoni

Muktasari:

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam  nchini Tanzania, Paul Makonda amesema anatamani kukutanishwa na watu wanaobishana kwenye mitandao ya kijamii kwa kuwa wanajadili mambo bila kuwa na uhalisia.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam  nchini Tanzania, Paul Makonda amesema anatamani kukutanishwa na watu wanaobishana kwenye mitandao ya kijamii kwa kuwa wanajadili mambo bila kuwa na uhalisia.

Makonda amesema hayo leo Ijumaa Februari 14, 2020 wakati akihojiwa katika kipindi cha 360 kinachorushwa na kituo cha televisheni cha  Clouds TV.

Watangazaji wa kipindi hicho,  Babbie Kabaye na Hassan Ngoma walimuuliza maswali mbalimbali likiwemo la wanaotumia mitandao ya kijamii kudai Makonda  anawasimanga kwa kusema wanafunzi ni masikini na wanasomeshwa na Rais John Magufuli, kuhoji  kama  anayewasomesha ni Rais au wanasoma kwa kodi za wananchi.

Serikali ya Awamu ya Tano ilianzisha utaratibu wa kutoa elimu ya awali, msingi na sekondari bila malipo.

Akijibu swali hilo Makonda amesema anahitaji kukutana na watu hao kwa kuwa wanazungumza mambo ambayo hawana uhalisia.

“Unajua tatizo lililopo ni moja, na ndio maana nataka siku moja mnitafutie wale watu wabishi, wale wanaojidai wanajua vitu halafu mnikutanishe nao, muandae kipindi kimoja kizuri, nileteeni.”

“Tukuletee wale watu wa Twetter,” aliuliza Ngoma na Mkaonda kujibu, “wote nileteeni, nileteeni. Nahitaji hawa watu kwa sababu  wengi wanajadili vitu kwa kusikia kwa sikio la tatu, uhalisia wa jambo hawana.”