Makonda akwepa kuzungumzia kupigwa ‘stop’ kuingia Marekani

Muktasari:

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amekwepa kuzungumzia kuziwa kuingia nchini Marekani kwa maelezo kuwa kuna siku atalizungumzia suala hilo.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amekwepa kuzungumzia kuziwa kuingia nchini Marekani kwa maelezo kuwa kuna siku atalizungumzia suala hilo.

 

Makonda ametoa majibu hayo leo Ijumaa Februari 14, 2020 wakati akihojiwa katika kipindi cha 360 kinachorushwa na televisheni ya Clouds, kutaka kutoulizwa masuala binafsi.

 

Februari Mosi, 2020 Marekani ilieleza kumzuia Makonda kuingia Marekani pamoja na mkewe, Mary Massenge na kwamba sababu ni tuhuma za kushiriki kukandamiza haki za binadamu.

 

Nchi hiyo ilieleza kuwa ukiukwaji wa haki za binadamu alioufanya jijini Dar es Salaam ni pamoja na kunyima watu haki ya kuishi, haki ya uhuru wa kujiamulia mambo na usalama wao.

 

Katika kipindi hicho ambacho Makonda alikuwa anazungumzia mambo mbalimbali  ya mkoa wa Dar es Salaam, aliulizwa kama tayari ameshapokea barua kutoka Marekani ya kumpiga marufuku kuingia nchini humo.

 

Akijibu sali hilo, Makonda amesema kuwa leo alifika katika kipindi hicho kuzungumzia masuala ya kiserikali si binafsi.

 

“Hapa nimekuja kama mkuu wa mkoa, subiri nikija binafsi tutajadiliana, nimekuja kama Serikali,” amesema

 

Amewataka watangazaji wa kipindi hicho, Babbie Kabaye na Hassan Ngoma kumtafuta wakati mwingine ambapo ataweza kuzungumza kuhusu masuala yanayomhusu yeye binafsi.