Makonda ataka ujenzi jengo la halmashauri Ubungo kukamilika Desemba 2019

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemuagiza Wakala wa Ujenzi nchini Tanzania (TBA) kukamilisha ujenzi wa jengo la Halmashauri ya Manispaa Ubungo Desemba 30, 2019 ili lianze kutumika.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemuagiza Wakala wa Ujenzi nchini Tanzania (TBA) kukamilisha ujenzi wa jengo la Halmashauri ya Manispaa Ubungo Desemba 30, 2019 ili lianze kutumika.

Makonda amesema kwa namna ujenzi huo unavyofanyika taratibu huenda ukakamilika Februari 2022 muda ambao hawezi kuvumilia.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya Manispaa ya Ubungo, Makonda amesema jengo hilo linatakiwa kukabidhiwa Desemba kwa sababu fedha za ujenzi zipo.

"Desemba sio mbali tusitafutane ubaya na pia tunataka ubora wa jengo kazi zangu zote nataka zikabidhiwe mwezi huo," amesema Makonda.

Awali mratibu wa mradi kutoka TBA,  Khalid Ng'oge amesema sababu za kuchelewa mradi huo ni utaratibu wa malipo ya fedha za ujenzi.

" Kwa sababu fedha zimepatikana tutakamilisha ujenzi huu, " amesema Ng'oge.

Mkurugenzi wa manispaa ya Ubungo, Beatrice Dominic amesema mpaka sasa zimetolewa Sh2. 2 bilioni za ujenzi.

"Limekamilika kwa asilimia 35 na fedha sio tatizo kama anavyosema," amesema Dominic.

Kutokana na hali hiyo, Makonda amewataka wajenzi hao kuwasiliana na ofisi yake wanapokumbana na changamoto ikiwamo za malipo.

Kwa sasa watumishi wa halmashauri ya manispaa ya Ubungo wanatumia jengo la muda lililojengwa Kibamba, karibu na ofisi zao mpya.