Moto ulioteketeza ghala kiwanda cha nguo Arusha wazimwa

Muktasari:

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limezima moto ulioteketeza  moja ya ghala la kuhifadhi pamba katika kiwanda cha nguo cha Sunflag mjini Arusha.

Arusha. Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limezima moto ulioteketeza  moja ya ghala la kuhifadhi pamba katika kiwanda cha nguo cha Sunflag mjini Arusha.

Moto huo ulioanza kuwaka leo  mchana Jumamosi Agosti 31, 2019, umezimwa saa 11 jioni huku viongozi wa kiwanda hicho wakiendelea kufanya tathmini ya hasara waliyoipata.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Jonathan Shana amethibitisha kutokea kwa moto huo na kubainisha kuwa kwa sasa umedhibitiwa.

“Bado hatujajua chanzo chake, maofisa wangu wanaendelea na uchunguzi,” amesema Shana

Baadhi ya wafanyakazi wa kiwanda hicho, John Minja na Rehema Issa wamesema waliona moshi ukitoka eneo la kuhifadhi vifaa.

“Tuliona moshi na baadaye viongozi walipiga simu kikosi cha Zimamoto waliofanikiwa kuuzima,” amesema Minja.

Viongozi wa kiwanda hicho wameahidi kutoa taarifa kamili baada ya moto huo kudhibitiwa maeneo yote.