Mwili wa Idd Simba kuzikwa kesho

Muktasari:

Mwili wa Waziri wa zamani wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Iddi Simba utazikwa kesho Ijumaa Februari 14, 2020 katika makaburi ya Mwinyimkuu Magomeni.

Dar es Salaam. Mwili wa Waziri wa zamani wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Iddi Simba utazikwa kesho Ijumaa Februari 14, 2020 katika makaburi ya Mwinyimkuu Magomeni.

Waziri huyo wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Tatu amefariki dunia leo Alhamisi Februari 13, 2020 katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) alikokuwa akipatiwa matibabu.

Mdogo wa marehemu, Ahmad Simba amelieleza Mwananchi kuwa mwili umehifadhiwa katika msikiti wa Mamuur Upanga.

“Kesho saa 5 asubuhi mwili utapelekwa katika msikiti wa Manyema kwa ajili ya kuswaliwa kisha makaburi ya Mwinyimkuu Magomeni. Tumeamua kumzika katika makaburi haya kwa sababu wazazi wetu wamehifadhiwa hapa,” amesema Ahmad.

Ahmad amesema kaka yake alizaliwa mwaka 1935 mjini na enzi za uhai wake aliwahi kuwa mtangazaji wa redio,  kufanya kazi  kwa nyakati tofauti Benki ya Dunia (WB) na Benki ya Maendeleo ya Afrika sambamba na kuwa mbunge wa Ilala kuanzia mwaka 1995 hadi 2005.