Mwili wa dereva taxi Arusha wakutwa umefungwa kamba

Kaimu kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Koka Moita

Muktasari:

  • Lembris Mollel (23), dereva taxi  mkazi wa Tengeru Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha amekutwa amekufa katika gari huku mikono yake ikiwa imefungwa na waya kwa nyuma.

Arusha. Lembris Mollel (23), dereva taxi  mkazi wa Tengeru Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha amekutwa amekufa katika gari huku mikono yake ikiwa imefungwa na waya kwa nyuma.

Akizungumza leo Jumanne Desemba 3, 2019 kaimu kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Koka Moita amesema mwili wa Mollel ukiwa na majeraha ulikuwa siti ya nyuma katika  gari aina ya Toyota Corolla lililokuwa limetumbukia mtoni katika mtaa wa Elikiroa kata ya Lemara.

Amebainisha kuwa polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo. Amesema mwili umehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru.

Katika tukio jingine, amesema mtoto wa miaka mitatu, Gifti Michael amekufa maji  baada ya kutumbukia kwenye shimo la kuhifadhi maji ya ujenzi.