Ndugai awapongeza Ngejela, Nape na Makamba kwa kuomba msamaha

Spika wa Bunge la Tanzania,  Job Ndugai leo Septemba 12,  2019 amewapongeza wabunge watatu wa CCM

Muktasari:

  • Spika wa Bunge la Tanzania,  Job Ndugai leo Septemba 12,  2019 amewapongeza wabunge watatu wa CCM kwa uamuzi wao wa kumuomba msamaha  Rais   John Magufuli.

Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania,  Job Ndugai leo Septemba 12,  2019 amewapongeza wabunge watatu wa CCM kwa uamuzi wao wa kumuomba msamaha  Rais   John Magufuli.

Wabunge hao ni Nape Nnauye (Mtama), William Ngeleja (Sengerema) na January Makamba (Bumbuli).

Akizungumza bungeni mara baada ya kipindi cha maswali na majibu, Ndugai amesema kitendo hicho ni cha kuigwa na wabunge wengine.

“Nawapongeza wabunge wangu watatu kwa jambo muhimu la kuomba radhi kwa Rais kwa yaliyotokea. Kwa binadamu wa kawaida kuomba radhi si jambo la kawaida na wengi wameshindwa kufanya hivyo,” amesema.

Amesema wabunge hao wamefanya jambo jema na zuri wanapaswa kupongezwa.

Ndugai pia amempongeza Rais Magufuli  kwa kuwasamehe wabunge hao, akisema kitendo hicho ni mfano wa kuigwa.

Juzi Nape alikwenda Ikulu Dar es Salaam kumuomba radhi Magufuli, akiwa ni mtu wa tatu kuomba msamaha kati ya wanachama sita waliohusishwa na sauti zilizosambaa mitandaoni zikizungumzia barua ya makatibu wa zamani wa CCM na pia hali ya chama kudhoofika na kumkejeli kiongozi mkuu huyo wa nchi.

Makamba, aliyevuliwa uwaziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais na Ngeleja aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini katika serikali iliyopita, ndio walikuwa wa kwanza kuomba radhi.