Rais Magufuli agawa majengo 11 ya Tanroads

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania, John Magufuli ameagiza nyumba 11 za Wakala ya Barabara Tanzania (Tanroads) katika mji mdogo wa Dumila Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro kuwa kituo cha afya Dumila.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli ameagiza nyumba 11 za Wakala ya Barabara Tanzania (Tanroads) katika mji mdogo wa Dumila Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro kuwa kituo cha afya Dumila.

Kiongozi mkuu huyo wa nchi ametoa agizo hilo leo Jumatano Novemba 20, 2019 wakati akizungumza na wakazi wa mji huo akiwa njiani kwenda Dodoma.

“Yale majengo yaliyokuwa ya Tanroads leo mnayachukua yanakuwa kituo cha afya, wataanza kuleta dawa kitakuwa kituo cha afya  ziko nyumba ngapi?”

“Zipo 11, kwa hiyo zote ninazikabidhi kituo cha afya cha Dumila” amesema Magufuli akisisitiza kuwa maagizo mengine atayatoa kwa wizara ya Afya ili kukamilisha kuwa kituo cha afya kwa kupeleka dawa na watendaji.

Amebadilisha matumizi ya nyumba hizo baada ya kuombwa na diwani wa Dumila, Deoglas Mgumila kuwa majengo hayo yanayotumiwa na Tanroads yaidhinishwe kuwa kituo cha afya.