Shaka adai upinzani hawana hoja

Morogoro. Katibu wa CCM mkoani Morogoro, Shaka Hamdu Shaka amesema kitendo cha baadhi ya vyama vya upinzani kudai tume huru ya uchaguzi ni kutapatapa baada ya kuona hawana uwezo wa kushinda uchaguzi mkuu mwaka huu.

Shaka ametoa kauli hiyo baada ya hivi karibuni vyama vya ACT-Wazalendo na Chadema kutaka kufanyika mabadiliko ili ipatikane tume huru ya uchaguzi itakayosimamia uchaguzi na kutoa haki kwa vyama vyote.

Jana akizungumza mjini hapa, Shaka alisema Rais John Magufuli amefanya kazi kubwa, hivyo wapinzani hawana nafasi ya kukishinda chama tawala.

“Kazi kubwa iliofanywa Rais Magufuli, imerudisha imani kwa wananchi, hivyo ni wazi vinajua hawawezi kupata kura katika uchaguzi mkuu. Vyama vya upinzani vimepoteza dira na mwelekeo wa kukubalika kwa wananchi,” alisema Shaka.

Alidai upinzani umeishiwa hoja, haulipui tena mabomu ya hujuma, ufisadi au kukosekana huduma za kijamii kwa wananchi na kwamba wanasubiri kuonewa huruma na wananchi.