TCU yavifutia usajili vyuo tisa Tanzania

Katibu mtendaji wa TCU, Profesa Charles Kihampa

Muktasari:

Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) imefuta hati za usajili wa vyuo vikuu vishiriki vitano, vyuo vikuu vitatu na chuo kikuu kishiriki kimoja

Dar es Salaam. Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) imefuta hati za usajili wa vyuo vikuu vishiriki vitano, vyuo vikuu vitatu na chuo kikuu kishiriki kimoja.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Januari 21, 2020 jijini Dar es Salaam katibu mtendaji wa TCU, Profesa Charles Kihampa amesema vyuo hivyo vimeshindwa kujirekebisha na hata vingepewa muda zaidi visingeweza.

Amesema vyuo vishiriki ni  Chuo kikuu kishiriki cha Askofu Mkuu Yakobo (AJUCO), Chuo Kikuu cha kumbukumbu ya Kardinali Rugambwa (CARUMUCo) na Chuo kikuu cha Theofilo Kisanji (Teku- Dar es Salaam),  Chuo kikuu cha Mtakatifu Yohana cha Tanzania kituo cha St Marks na Chuo kikuu cha Jomo Kenyatta cha Kilimo tawi la Arusha (JKUA).

"Kufuatia mashauriano na maombi yaliyofanywa na wamiliki wa vyuo na tume katika kikao chake cha 97 kilichofanyika Januari 20, 2020 imeridhia maombi ya wamiliki hao kusitisha utoaji wa mafunzo, hivyo tume imefuta hati za usajili wa vyuo hivyo vishiriki na kuvifutia vibali,” amesema Profesa Kihampa.

TCU pia imefuta hati za usajili wa vyuo vitatu ambavyo ni Chuo kikuu cha Josiah Kibira (Kagera), Mount Meru (Arusha), IMTU (Dar es Salaam). Chuo kikuu kishiriki kilichofutiwa usajili ni  Chuo Kikuu cha Bagamoyo (Pwani).

"Licha ya tume kutoa ushauri na mafunzo ya namna mbalimbali za kuboresha mazingira ya kufundisha na kufundishia pamoja na muda wa kufanya maboresho kwenye maeneo mbalimbali kwa zaidi ya miaka mitatu, baadhi ya vyuo havikufanikiwa, " amesema Profesa Kihampa.

Amesema kati ya vyuo 19 vilivyotakiwa kufanya marekebisho, vyuo vinane vilifanikiwa na kuruhusiwa kuendelea na udahili.