VIDEO: Makonda: Ninahujumiwa

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amelalamika kuhujumiwa na baadhi ya watendaji wa halmashauri katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya jiji.

Makonda alisema hayo jana katika kikao na watendaji wa wilaya na kata, ikiwa ni siku mbili baada ya Rais John Magufuli kuonyesha kutoridhishwa na ufuatiliaji wake wa miradi ya maendeleo, akitoa mfano wa machinjio ya Vingunguti na ufukwe wa Coco.

Jana, Makonda alisema kuna baadhi ya watendaji wanamchongea na ili kazi ziende ameamua kuanza kuzunguka na maofisa wa Jeshi la Polisi katika miradi hiyo ili anapokuta mambo hayaendi arudie tena mtindo wa kuwaweka mbaroni.

Makonda alisema kitendo cha baadhi ya watendaji kusambaza vikaratasi vyenye ujumbe kuwa hawamuelewi utendaji wake wa kazi, kinamsikitisha kwa kuwa amekuwa akifanya juhudi katika kujenga mawazo ya kuboresha miradi ya maendeleo.

“Na kwa sababu mheshimiwa Rais anaendeleza kusamehe watu na mimi sina mpango wa kuwashughulikia, nitaendelea kuwasamehe,” alisema.

“Ninajua mnavyonihujumu na mnashirikiana na baadhi ya viongozi wenzangu ninaowafahamu. Na mimi nitaanza kuwachongea kuanzia sasa,” alisema Makonda.

Wasaidizi wake ndani ya mkoa ni wakuu wa wilaya, mkurugenzi wa jiji na wa wilaya na makatibu tawala, ambao mamlaka za uteuzi ziko juu yake, huku akiwa na mamlaka ya kuwaapisha na kusimamia utendaji wao, ingawa hana mamlaka ya kuwaadhibu.

Kwa undani wa habari hii pata nakala ya Gazeti la Mwananchi, Septemba 26,2019.