Vikwazo 175 visivyo vya ushuru vyapatiwa ufumbuzi EAC.

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imesema katika kipindi cha miaka 10 iliyopita vikwazo vya biashara visivyo vya kiushuru (NTBs) 174 vimeondolewa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kutokana na juhudi mbalimbali.

Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesema katika kipindi cha miaka 10 iliyopita vikwazo vya biashara visivyo vya kiushuru (NTBs) 174 vimeondolewa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kutokana na juhudi mbalimbali.

Hayo yameibainishwa leo Jumanne Oktoba 8, 2019 na mkurugenzi msaidizi wa idara ya biashara wa Wizara ya Viwanda na Biashara,  Sekela Mwaisera katika mkutano wa jumuiya za wafanyabiashara na kuhusu NTBs.

“Kutokana na juhudi mbalimbali zilizofanywa  kwa miaka 10 iliyopita tumefanikiwa kuondoa takribani NTBs 174 ambazo ni sawa na asilimia 75 ya vikwazo vilivyokuwa vikilalamikiwa na wafanyabiashara,” amesema Mwaisera katika hotuba yake aliyoisoma kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara,  Stella Manyanya.

Mwaisera amesema Serikali ya Tanzania inaendelea kutatua changamoto na kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara ikiwa ni pamoja na miundombinu ya umeme, bandari, barabara, reli ya kisasa na kufufua Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).

“Baada ya kukamilika kwa miundombinu hii itatoa fursa za kuchochea kasi ya ufanyaji wa biashara hapa nchini na kukuza uwekezaji katika maeneo mbalimbali kwani gharama za uendeshaji zitapungua,” amesema Mwaisera.