Wazalendo Kwanza kuhamasisha uandikishaji Daftari la Wapigakura

Steve Mengere maarufu Steve Nyerere

Muktasari:

Taasisi ya Wazalendo Kwanza imejitolea kuhamasisha  uandikishaji wa Daftari la Wapigakura kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 24, 2019.

Dar es Salaam. Taasisi ya Wazalendo Kwanza imejitolea kuhamasisha  uandikishaji wa Daftari la Wapigakura kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 24, 2019.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Septemba 10, 2019 mwenyekiti wa taasisi hiyo, Steve Mengere maarufu Steve Nyerere amesema taasisi hiyo itafanya kazi hiyo Wilaya ya  Kinondoni.

Steve amesema katika uhamasishaji huo watatoa  elimu na kuburudisha na kuongeza kuwa wasanii wana nafasi kubwa katika kuwaelewesha wananchi umuhimu wa kushiriki katika uchaguzi huo ngazi ya mitaa.

"Kinondoni ndio Dar es Salaam tuna kila sababu ya kuwahamasisha wananchi kujitokeza kupiga kura kwani viongozi wa Serikali za Mitaa ni wa muhimu kwetu," amesema.

Makamu mwenyekiti wa taasisi hiyo, Luiza Mbutu amesema viongozi wa Serikali za mitaa ni muhimu kuwachagua kwa kuwa hao ndio wanaowasilisha kero za mwananchi katika ngazi ya wilaya na baadaye Mkoa na Taifa.

Kwa upande wake msanii Dude amesema wananchi kujitokeza kupiga kura kutasaidia kuondoa malalamiko ya kuchaguliwa viongozi wabovu na kubainisha kuwa wengine hubaki nyumbani siku ya kupiga kura na baadaye kulalamikia uongozi uliopo kuwa sio chaguo lao.