VIDEO: Wanandoa raia wa China mahakamani kwa kutaka kumpa rushwa kamishna wa TRA

Watuhumiwa wanao daiwa kutoa rushwa kwa kamishna wa TRA  Zeng Ronglan  (kushoto) ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Ronglan  ITL  INTL  kushoto mwanaume akiwa na mwezake  OU YA kulia wote ni wakazi wa Mafinga Iringa wakitoka katika mahakama ya hakim mkazi kisutu kusomewa shitaka lao la Rushwa Picha na  Omar Fungo

 

 

 

Muktasari:

Zheng Rongman na mkewe, Ou Ya wote raia wa China wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa tuhuma za kutoa rushwa ya Dola 5,000 za Kimarekani sawa na Sh11.5 milioni kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini Tanzania (TRA), Dk Edwin Mhede.

Dar es Salaam. Zheng Rongman na mkewe, Ou Ya wote raia wa China wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa tuhuma za kutoa rushwa ya Dola 5,000 za Kimarekani sawa na Sh11.5 milioni kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini Tanzania (TRA), Dk Edwin Mhede.

Rongman ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Ronglan Intl Industry and Trade Co Ltd na mkewe wamekiri kutaka kutoa rushwa kwa bosi huyo wa TRA. Wanandoa hao ni  wakazi wa Wilaya ya Mafinga mkoani Iringa.

Wamefikishwa mahakamani leo Jumanne Februari 25, 2020  na kusomewa shtaka moja la kutoa rushwa.

Akiwasomewa hati ya mashtaka wakili wa Takukuru, Ipyana Mwakatobe amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa washtakiwa wanakabiliwa na kesi ya jinai namba 30/2020.

Mwakatobe amesema washtakiwa wanadaiwa kutenda kosa hilo  Februari 24, 2020 makao makuu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), jijini Dar es Salaam.

Imedaiwa kuwa siku ya tukio  walitoa rushwa kwa Dk Mhede ili kumshawishi iwasaidie kampuni yao isilipe kodi ya Sh1.3 bilioni.

Baada ya kusomewa shtaka lao, walikiri kutenda kosa hilo na

Hakimu Shaidi amesema kesi hiyo itaendelea kesho kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali.

Pia Hakimu Shaidi ameutaka upande wa mashtaka kumleta mkalimani kwa ajili ya mshtakiwa wa kwanza ambaye hajui vizuri lugha ya Kiingereza.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 26, 2020 itakapoendelea na washtakiwa wamerudishwa rumande.