Harmonize, Killy na Cheed kumalizana Jumatatu
Muktasari:
Mmiliki wa lebo ya Konde Music Worldwide, Rajab Abdul maarufu Harmonize na wasanii Ally Omar, (Killy) na Rashid Mganga (Cheed) wamekubaliana kuvunja mkataba rasmi Jumatatu Oktoba 24, 2022
Dar es Salaam. Mmiliki wa lebo ya Konde Music Worldwide, Rajab Abdul maarufu Harmonize na wasanii Ally Omar, (Killy) na Rashid Mganga (Cheed) wamekubaliana kuvunja mkataba rasmi Jumatatu Oktoba 24, 2022
Killy na Cheed walijiunga rasmi na lebo hiyo Septemba 2020 wakitokea King’s Music inayomilikiwa na msanii Alikiba
Akizungumza leo Ijumaa Oktoba 21, 2022 baada ya kumaliza kwa kikao kati ya wasanii hao Ofisa Sanaa Mwandamizi wa Baraza la Sanaa Taifa (Basata), Abel Ndaga amesema Jumatatu pande zote mbili zinakutana kuvunja mkataba rasmi kwa maandishi.
“Jumatatu wanavunja mkataba rasmi ili kila mmoja aendelee na majukumu yake, kwani upande mwingine wakina Cheed walikuwa wanashindwa kufanya chochote kwa kuwa mkataba ulikuwa unawabana kisheria” amesema Ndaga ambaye pia ndio alikuwa Mwenyekiti wa kikao hicho.
Kwa upande wake Meneja wa wasanii cheed na Killy, Saty Sembe amesema watamalizana na lebo hiyo siku ya Jumatatu katika ofisi ya Basata kama kikao kilivyoamua.
"Siku hiyo kati ya mambo tutakayomalizana ni kutupa barua rasmi, kuwalipa wasanii wangu malipo ya Sh10 milioni kila mmoja pia kuziachia digital platform zetu zote ambazo zilikuwa chini ya lebo hii," amesema Sembe.
Naye, mwanasheria wa Harmonize, Musa Nassoro alipotafutwa na Mwananchi Digital alieleza kuwa Harmonize au meneja wa msanii huyo Chopa ndio wanaweza kulizungumzia sakata hilo.
"Mtaambiwa tu nini kimefikiwa na Harmonize au Chopa ambaye ni meneja, mimi nisingependa kuliongelea hilo kwa kuwa sio mzungumzaji zaidi ya kuwapa taraifa ya tulichokubaliana kikaoni,"alisema Nassoro.