Mahakama yaamuru aliyetolewa group la Whatsapp arudishwe
Muktasari:
- Mahakama mjini Kampala nchini Uganda, imemuamuru kiongozi wa kundi la whatsapp (Admin) kumrudisha kwenye kundi hilo baada kumtoa mshirika mmoja bila ridhaa yake baada ya kuhoji kuhusu fedha za michango.
Uganda. Jumatatu wiki hii, Hakimu Mwandamizi katika Mahakama ya Mwanzo huko Makindye, Kampala, Igga Adiru, alimwamuru Allan Asinguza ambaye ni mlalamikiwa kumrudisha Herbert Baitwababo katika kundi la whatsapp lilitwalo Buyanja Roots ambamo alikuwa mshirika awali.
Baitwababo alisema, Asinguza alitengeneza kundi la Whatsapp kwa watu wa eneo la Buyanja ambalo lilikua na lengo la michango ya kijamii na shughuli za kujitolea na kusaidiana kipindi cha majanga.
“Mimi kama mshirika wa kundi hilo, tulianzisha wazo la kutengeneza chama na tukakubaliana kutoa Sh30,000 kama ada mtu kujiunga na kuwa mwanachama, na mimi nilitoa ada hiyo ambapo taarifa zote za chama zilitolewa na kujadiliwa kupitia kundi hilo,” alisema Baitwababo.
Baitwababo alieleza kuwa Mei 16, 2023 akiwa mwanachama aliyesajiliwa wa chama hicho, alimwandikia barua Asinguza kutaka kujua kuhusu fedha zilizokusanywa kutoka kwa wanachama waliosajiliwa tangu mwaka wa 2017 lilipoanzishwa.
Alisema kwamba baada ya kumuandikia barua kiongozi huyo wa kundi ndipo alipoamua kumtoa kwenye kundi hilo mnamo Mei 17, 2023 ambapo kwa taratibu za kundi hilo, kuhoji michango ni kosa na ndipo Baitwababo alipoamua kutinga mahakamani kutoa malalamiko yake na mahakama kuamuru arudishwe.