Museveni akanusha kulazwa ICU, awashukia Wakenya

Muktasari:

  • Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya ya Uganda, Diana Atwine, afichua jinsi Museveni alivyogundulika kuwa na ugonjwa wa Uviko-19 baada ya kupata dalili ya mafua, naye Rais huyo akitumia ukurasa wake rasmi wa Twitter kukanusha madai kwamba alilazwa ICU.

Uganda. Rais wa Uganda, Yoweri Museveni amewataka wananchi wa Taifa hilo kutupilia mbali anaouita uzushi wa kuwa amefariki kutokana na Uviko-19.

Hatua hiyo inakuja baada ya siku kadhaa kupita tangu Rais huyo atangaze kukutwa na ugonjwa huo.

Kiongozi huyo wa muda mrefu siku ya Jumanne Juni 13, 2023 alitumia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii Twitter, kuwataarifu watu kutupilia mbali uvumi wa kifo chake kutokana na virusi hivyo.

Kwa mujibu wa kituo cha habari ‘Tuko’ wameeleza kwamba, Rais huyo ambaye amekuwa madarakani tangu Januari 1986 amesema tangu apate maambukizi hayo ni siku tano zimepita na afya yake inazidi kuimarika.

"Takriban siku mbili (2) zimepita tangu nitoe taarifa kuhusu vita yangu na ugonjwa wa uviko-19. Kwa siku mbili za kwanza (Jumanne na Jumatano), nilikua na homa kali ya mafua. Nilipata tu usingizi siku ya Alhamisi na maumivu ya kichwa kidogo usiku. Hii ilikuwa hadi Ijumaa," Museveni

Mkuu huyo wa nchi pia aliwalaumu baadhi ya wananchi kutoka nchi ya jirani ya Kenya kwa kusambaza uvumi kuhusu hali ya afya yake.

"Niliona watu wachache nafikiri ni kutoka Kenya wakisema niko ICU (Chuma cha wagonjwa mahututi) sasa kama ningekuwa ICU serikali ingeijulisha nchi, kwani kuna nini cha kuficha,”amesema Museveni.

Jinsi Museveni alivyogunduliwa na UVIKO-19

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya ya Uganda, Diana Atwine, amesema Museveni aligunduliwa na virusi hivyo baada ya kupata dalili za mafua. Hata hivyo pamoja na kukumbana na changamoto hiyo Museveni bado anatekeleza majukumu yake rasmi ya kuendesha nchi kama kawaida.