Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Serikali ya Venezuela yajitetea ilivyoratibu uokoaji, vifo vya tetemeko vikifikia 2,295

Muktasari:

  • Kwa mujibu wa Serikali ya Venezuela na mashirika ya misaada ya kimataifa, matetemeko mawili ya ardhi yamesababisha vifo 2,295, huku mjadala ukiibuka kuhusu kasi ya uokoaji na msaada kwa waathirika

Dar es Salaam. Serikali ya mpito ya Venezuela imejitetea dhidi ya ukosoaji wa ndani na kimataifa kuhusu namna ilivyoshughulikia uokoaji kufuatia matetemeko mawili ya ardhi yaliyolikumba taifa hilo na kusababisha vifo vya watu 2,295.

Kwa mujibu wa taarifa ya serikali ya Venezuela iliyotolewa kupitia mkutano na waandishi wa habari mjini Caracas, Rais wa mpito, Delcy Rodríguez amenukuliwa na Deutsche Welle (DW), kisema serikali ilianzisha hatua za dharura ndani ya saa chache baada ya majanga hayo kutokea, ikiwamo kuunda Kamandi ya Pamoja ya kusimamia uokoaji.

Kwa mujibu wa Shirika la Huduma za Dharura za Venezuela (Civil Protection Service), vikosi vya uokoaji vilianza mara moja kufanya kazi katika maeneo yaliyoathirika, yakijumuisha miji mikubwa na maeneo ya milimani ambako majengo yaliporomoka na miundombinu kuharibiwa vibaya.

Hata hivyo, mashirika ya misaada ya kimataifa, kama yalivyoripotiwa na Shirika la Msalaba Mwekundu (Red Cross) katika taarifa yake ya awali, yameeleza kuwa mwitikio wa serikali ulikuwa wa polepole, yakieleza kuchelewa kwa chakula, dawa na vifaa vya uokoaji, pamoja na uhaba wa mitambo ya kuchimba vifusi katika baadhi ya maeneo.

Kwa mujibu wa ripoti ya waokoaji wa kujitolea walioko mashinani iliyonukuliwa na vyombo vya habari vya kimataifa, shughuli za uokoaji zilikuwa zikiendelea kwa kusuasua kutokana na miundombinu kuharibiwa na ukosefu wa uratibu wa haraka katika saa za mwanzo za tukio.

Hata hivyo, katika mkutano wake na waandishi wa habari ulioripotiwa na shirika la habari la serikali (Venezolana de Televisión), Rais Rodriguez amekanusha madai hayo, akisema serikali ilichukua hatua za haraka na za kitaasisi mara baada ya tukio.

"Jambo la kwanza tulilofanya, saa chache tu baada ya tukio hilo, lilikuwa ni kuanzishwa kwa Kamandi ya Pamoja ya Wakuu wa Majeshi ili kushughulikia dharura hii iliyosababishwa na janga la asili," amesema.

Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Ulinzi wa Raia (National Civil Protection Authority), Meja Jenerali Zurbarán wa Walinzi wa Kitaifa wa Bolivari aliteuliwa kuratibu shughuli zote za uokoaji na usambazaji wa misaada katika maeneo yaliyoathirika.

Taasisi hiyo imeripoti hadi kufikia Jumatano, idadi ya waliopoteza maisha ilifikia watu 2,295, huku ikiweka tahadhari kuwa huenda ikaongezeka kadri shughuli za uokoaji zinavyoendelea katika vifusi vya majengo yaliyoporomoka.

Kwa upande wake, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuratibu Misaada ya Kibinadamu (OCHA) limeripoti kuwa bado kuna upungufu mkubwa wa vifaa vya uokoaji katika baadhi ya maeneo ya mbali, hali inayochelewesha kufikia manusura wanaoweza kuwa chini ya vifusi.

Wakati serikali ikisisitiza kuwa majibu yake yalikuwa ya haraka na yaliyoratibiwa kupitia mfumo wa kijeshi na dharura, mashirika ya kiraia na baadhi ya wahudumu wa uokoaji wanasema bado kuna changamoto kubwa za uratibu na usambazaji wa msaada.

Mpaka sasa, serikali ya Venezuela inaendelea kusimamia operesheni za uokoaji huku mjadala ukiendelea kuhusu ufanisi wa majibu ya awali na ukubwa halisi wa athari za janga hilo nchini humo.